Saturday, June 25, 2016

Rais Magufuli azindua Mpango mkakati wa kupunguza uhalifu

Rais DK. John Pombe Magufuli leo amezindua mpango mkakati wa kupunguza uharifu nchini huku akilitaka jeshi la polisi kuwasaka kwa udi na uvumba majambazi nchini kote na kisha kuwachukulia hatua stahiki.
Akizindua mpango huo Rais Dk, Magufuli amesema mpango huo wa miaka mitatu ambao utaanza kutekelezwa katika mkoa wa kipolisi wa Kinondoni Julai Mosi, utafanikiwa tu endapo wananchi watashirikiana kikamilifu na jeshi la polisi , huku akimtaka mkuu wa jeshi la polisi nchini Ernest Mangu kuhakikisha analisafisha jeshi lake kwa kuwachukulia hatua ikiwemo kuwafukuza askari wote watakaobainika wanakwenda kinyume na maadili ya kazi zao.
Wakizungumza katika uzinduzi wa mpango huo ambao lengo lake kuu ni kukomesha uhalifu nchini ,wafadhili wakuu wa mpango huo wakiwemo benki ya CRDB ambao wametoa zaidi ya shilingi milioni 320 kujenga kituo cha kisasa cha mawasiliano pamoja na benki ya NMB ambao nao pia wamejenga vituo vya polisi viwili vinavyohama , wamesema ulinzi na usalama ni jukumu la kila mwananchi na kwamba bila usalama na amani hakuna shughuli yoyote ya kijamii na kiuchumi inayoweza kuendelea.
Awali Rais Magufuli alizindua kituo cha kisasa cha mawasiliano kilichopo kituo kikuu cha polisi kanda maalum ya Dar es salaam ambapo akiwa katika viwanja vya biafra alitembelea mabanda mbalimbali ya polisi ili kujifunza zaidi juu ya mpango huo wa kuboresha usalama wa raia.