Friday, May 6, 2016

TRA imefanikiwa kukusanya kiasi hiki katika mwezi April

TRA
Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) imefanikiwa kukusanya shilingi Trilioni 1.035 ambayo ni sawa na asilimia 99.5 ya lengo la kukusanya shililingi Trilioni moja na bilioni 40 (Trilioni 1.040) katika mwezi April.
Ambapo makusanyo kwa kipindi cha miezi kumi kuanzia Julai 2015 hadi April 2016 jumla ya shilingi Trilioni 10.92 sawa na asilimia 99 ya lengo la shilingi Trilioni 11.02 katika lengo yamekusanywa.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam kuhusu mwenendo wa makusanyo ya mapato, Kamishna mkuu wa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania, TRA,  Alphayo Kidata, amesema TRA inaendelea na jitihada kuhakikisha inafikia na kuvuka lengo la makusanyo kwa mwaka wa fedha 2015/2016 licha ya kuwepo na changamoto mbalimbali inazokabiliana nazo.
Amesema kwa kipindi cha miezi miwili iliyobaki TRA imedhamiria kukusanya zaidi ya shilingi Trilioni 1.4 ili kufikia na kuvuka lengo la mwaka 2015/2016 ambalo ni shilingi trilioni 12.3, huku wakiendelea kudhibiti wafanyabiashara wanaokwepa kutumia mashine za kielektroniki za kodi (EFD’S) kwa kuwakamata na kuwatoza faini au kuwafikisha mahakamani.
Mpaka sasa wafanyabiashara zaidi ya 300 nchi nzima wamekamatwa na kutozwa faini ya shilingi milioni 746 kwa makosa ya kutotoa risiti, kutoa risiti yenye bei pungufu na kutotumia mashine za kielektroniki, huku baadhi ya wafanyabiashara miongoni mwa waliokamatwa walihukumiwa kifungo au kulipa faini.